GLOBALWISE SOFTNET & GRAPHIC DESIGNER: Jairo apelekwa likizo, CAG kumchunguza

Friday, July 22, 2011

Jairo apelekwa likizo, CAG kumchunguza

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, amepewa likizo kuanzia leo ili kupisha uchunguzi juu ya tuhuma zinazomkabili na kupata ukweli kabla ya hatua zingine kuchukuliwa.

Katibu Mkuu Kiongozi, Phillemon Luhanjo, alisema jana mjini Dodoma kwamba, yeye ndiye mwenye mamlaka ya nidhamu na kwa kuwa tuhuma zinazomhusu Jairo ni za fedha, amemteua Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kumpa siku 10 afanye uchunguzi wa awali.

Luhanjo alisema, ndani ya siku kati ya mbili na tatu, atakuwa amemteua mtu wa kukaimu nafasi hiyo, wakati Jairo akiwa katika likizo hiyo ambayo ni ya malipo. “Siku mbili, tatu mtasikia nani nimemteua,” alisema Luhanjo.

Katibu Mkuu Kiongozi alitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari na kusema tuhuma dhidi ya Jairo ni nzito hali ambayo imemlazimu kuamua aende likizo licha ya kwamba Sheria namba 8 ya mwaka 2002 na kanuni zake za utumishi wa umma za mwaka 2003, inaruhusu mtuhumiwa kuendelea na kazi wakati uchunguzi ukifanywa.

No comments: